Mkataba ni makubaliano baina ya
watu au pande kadhaa yenye nguvu kisheria. Mkataba unaweza kuwa wa maandishi, mdomo au vitendo.
Mkataba wa maandishi ni aina ya
makubaliano yanayoweza kufikiwa na kuwekwa katika mfumo wa kimaandishi. Katika
aina hii ya mkataba ni vyema kabisa mambo ya msingi katika makubaliano yakajumuishwa
ndani. Kanuni za kiuandishi ni sharti zizingatiwe ili kuondoa utata unaoweza
kujitokeza mbeleni kwenye tafsiri.
Mkataba wa mdomo unaweza kufanywa
kwa maneno ya mdomo. Kwa mfano unapokwenda dukani kwa Mangi mtaani kununua
bidhaa fulani fulani za rejareja huwa hamuandikishiani bali mnakubaliana kwa
njia ya mdomo.
Lakini pia tunapopanda daladala ili kusafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine hatuandikishani mkataba na makondakta bali huwa makubaliano yanafanyika kwa njia ya mdomo kwamba anakufikisha sehemu fulani kituoni unashuka halafu unamlipa nauli. Hii ni baadhi ya mifano kadhaa ninayoweza kukupa kuhusiana na aina hii ya mkataba.
Lakini pia tunapopanda daladala ili kusafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine hatuandikishani mkataba na makondakta bali huwa makubaliano yanafanyika kwa njia ya mdomo kwamba anakufikisha sehemu fulani kituoni unashuka halafu unamlipa nauli. Hii ni baadhi ya mifano kadhaa ninayoweza kukupa kuhusiana na aina hii ya mkataba.
Mkataba wa vitendo ni mkataba
amabao unaoweza kufanywa kwa njia ya matendo. Kwa mfano msambazaji wa mchele wa
jumla kama kwa kawaida huwa analeta gunia kadhaa za mchele na anamwachia muuzaji hafafu muuzaji
akimaliza kuuza anamlipa yule msambazaji japokuwa hawakuandikishiana popote makubaliano
yale yatakuwa na nguvu kisheria kwani mkataba ule tutauita mkataba au makubaliano ya vitendo (implied
contract).
Ni upi mkataba wenye nguvu kisheria?
Maelezo ya hapo juu yanaweza
yakawa ni makubaliano tu na sio mkataba. Ijulikane ya kwamba mikataba yote ni
makubaliano ila sio makubaliano yote ni mikataba isipokuwa yamekidhi vigezo vya
kimkataba. Vigezo hivyo vimewekwa na sharia
ya mikataba ya Tanzania kwa jina la The Law of Contract Act, [R.E 2002]. Kwenye
kifungu cha 10 cha sharia hiyo kinataja baadhi ya vigezo ambayo ni lazima
yawepo kwenye makubaliano fulani ili yaweze kuwa mkataba.
Vigezo hivyo ni kama vile lazima
kuwe na makubaliano huru baina ya pande zinazohusika katika mkataba. Na
makubaliano hayo hayapaswi kufikiwa kwa kushawishiwa na rushwa, kulazimishwa au
nguvu.
Lakini pia wahusika wa mkataba ni
sharti wawe na uwezo kisheria wa kuingia mkataba. Uwezo wa kisheria
unaohitajika ili mtu aweze kuingia mikataba ni kama vile kutimiza umri wa miaka
kumi na minane (18) au zaidi na asiwe na tatizo la akili wakati wanaingia makubaliano
hayo kwa kiasi ambacho kitaathiri kuingiwa kwa mkataba.
Mkataba pia usiwe na lengo linalokwenda
kinyume cha sharia au sera za nchi. Huwezi kufanya mkataba wa kuuziana bangi au
dawa za kulevya au kuua mtu au kuuza mwili kingono ukadhani utakuwa na nguvu
kisheria, haitowezekana kamwe kwani lengo lake linakwenda kinyume kabisa na
sheria au sera za nchi.
Kigezo kingine ni lazima katika
mkataba kuwe na mabadilishano ya kitu kwa kitu yanayoruhusiwa na sharia (a
lawful consideration). Kwa mfano unapokwenda kununua nyumba kwa kiasi cha
shilingi milioni kumi, tunasema hiyo milioni kumi ni consideration ya thamani
ya nyumba. Hivyo ni baadhi ya vigezo vichache vinavyotakiwa ili makubaliano
yawe mkataba.
Ndugu msomaji wangu pengine
unaweza kujiuliza ni nini basi maana ya makubaliano? Na ni kwanini sio makubaliano
yote yanaweza kuwa na nguvu kisheria au kuitwa mkataba? Nitalijibu swali hili
kwa mifano.
Tuchukulie unae mtoto anasoma kidato cha nne na ukamuahidi simu aina ya SAMSUNG NOTE 5 endapo ataweza kufaulu mitihani yake ya kidato cha nne, ni wazi kabisa haya ni makubaliano tu kati ya mzazi na mwanawe na mtoto hatoweza kwenda kufungua shauri mahakamani kumshtaki mzazi wake kwa sababu hayajaweza kukidhi baadhi ya vigezo vinavyotakiwa na sheria ili yaweze kuwa mkataba.
Tuchukulie unae mtoto anasoma kidato cha nne na ukamuahidi simu aina ya SAMSUNG NOTE 5 endapo ataweza kufaulu mitihani yake ya kidato cha nne, ni wazi kabisa haya ni makubaliano tu kati ya mzazi na mwanawe na mtoto hatoweza kwenda kufungua shauri mahakamani kumshtaki mzazi wake kwa sababu hayajaweza kukidhi baadhi ya vigezo vinavyotakiwa na sheria ili yaweze kuwa mkataba.
Mfano wa pili ni mume anaweza
akamuahidi mkewe kumnunulia gari katika sherehe ya kukumbuka siku yake ya
kuzaliwa, haya pia ni makubaliano yasiyoweza kufikia uwezo wa kuitwa mkataba
kwani mume akishindwa kutimiza alichokiahidi mkewe hawezi kumshtaki mumewe kwa
kuvunja mkataba kwani huo haujatimiza vigezo vya kuitwa mkataba.
Jinsi ya kuandaa mkataba wa biashara
Haya ni baadhi ya mambo yanayopaswa
yawepo wakati unaandika mkataba wa biashara. Nomba ijulikane kwamba hakuna namna
maalumu ya kuandika (draft) mkataba isipokuwa yapo mambo muhimu yanayoyakiwa
yawepo katika mkataba:
1. Kichwa cha mkataba.
Huwa kinatangulia mwanzo wa mkataba
kabla ya mambo yote. Kichwa cha mkataba kinaweza kuwekwa juu kabisa ya mkataba
katikati kama ukipenda. Kichwa cha mkataba kinatakiwa kueleza mkataba huo
unahusiana na nini kwa ufupi sana. Kinaposomwa kichwa cha mkataba picha ya
mkataba mzima inatakiwa ionekane bila hata ya kuusoma ndani. Mfano inaweza
ikawa hivi MKATABA WA MAUZIANO YA NYUMBA
2. Taja majina ya wahusika wa mkataba
Baada ya kichwa cha mkataba
unaweza ukaandika majina ya pande zinazohusika katika mkataba. Kumbuka sio kila
mtu anatakiwa kuingia kwenye mkataba kama nilivyokwisha kudokeza. Kwa mfano, muunganiko
wa kichwa cha mkataba na majina ya pande husika zinaweza kuwa katika muonekano
ufuatao:
MKATABA WA MAUZIANO YA SHAMBA
kati ya
COMFORT M. NGOWI (wa S.L.P 54 Marangu,
ambapo kwenye mkataba huu atajulikana kama ‘Muuzaji’)
na
FAITH M. NGOWI (wa S.L.P 432 Mabibo,
ambapo katika mkataba huu atajulikana kama ‘Mnunuaji’)
3. Tarehe na mahali mliposainishana mkataba
Hii pia ni shehemu muhimu sana.
Ni vyema tarehe ya siku mnayosainishiana mkataba ikawepo bila kusahau mahali.
Inaweza ikawa ni mji au wilaya. Mfano: Mkataba huu umefungwa hapa DAR ES SALAAM
leo Tarehe 21.08.2017.
4. Siku ya mkataba utakapoanza na kufikia ukomo
rasmi
Kama mkataba unategemewa kuanza
siku tofauti na ile ambayo wahusika wamesainishiana basi ni sharti kuwepo
kifungu kinachoonyesha hivyo. Hii inatokea pale wahusika wa mkataba hawataweza
kuonana siku za usoni hivyo mnaweza kusainishana mkataba tarehe fulani halafu mnaweka
na kifungu kinachoonyesha siku utakapoanza rasmi.
Kwa kuongezea tu kama mkataba una
siku ya kufikia ukomo ni vyema tarehe ikaandikwa japokuwa hii sio muhimu sana
kwani zipo njia nyingine zinazoweza kuufikisha mkataba kwenye ukomo.
5. Kiwango cha fedha kinachotumika
Kiwango cha fedha kinachotumika
katika biashara ni lazima kitajwe. Kwa mfano: Unaweza kuandika hivi ‘Kwamba
muuzaji kamuuzia mnunuaji nyumba iliyoko Mabibo yenye namba Mabibo- Mwananchi
plot b/480 Ubungo kwa kiasi cha Shilingi za KItanzania Milioni 800.
6. Kitu kinachohusika katika biashara
Ni lazima mkataba utaje ni kitu
gani kinachohusika katika biashara mnayoiingia mkataba. Ni vyema ukaweka
taarifa zote ambazo unadhani ni muhimu zinazohusiana na kitu hicho.
Rejea kwenye mfano nilioutoa hapo
juu ‘Nyumba’ ndio kitu kinachohusika katika biashara. Na kama ambavyo tulivyoweza
kuona taarifa kuhusiana na nyumba hiyo zimetolewa kama vile namba ya kiwanja
pamoja na sehemu kilipo. Hii itasaidia kuondoa utata pindi litakapotokea tatizo
baadae.
7. Namna malipo yatakavyofanyika
Je unataka njia gani itumike
katika kufanya malipo? Je ni kwa njia ya Benki au Mkono au M-Pesa au Tigopesa?
Je unataka malipo yafanyikeje, yote kwa pamoja au kidogo kidogo? Je unataka
ulipwe kwa kutumia pesa ya kitanzania au kigeni? Yote haya unaweza ukayaweka
kwenye mkataba kama sehemu ya makubaliano yenu.
8. Sehemu ambayo mngependa mgogoro ushughulikiwe endapo
utatokea
Hapa mnaandika ni wapi mngependa
mgogoro ushughulikiwe pindi utakapotokea. Je mtapenda kupeleka mgogoro wenu
mahakamani au kwenye mabaraza ya usuluhishi? Kama mmoja wenu ni raia wa kigeni
je mngependa iwe nchi gani yenye mamlaka ya kushughulikia mgogoro wenu? Kumbuka
kama mmekubaliana katika mkataba mgogoro utakapotokea upelekwe sehemu fulani
hamna atakayeweza kufanya vinginevyo nje ya makubaliano yanu.
9. Sheria ambayo mngependa itumike kusimamia
mkataba wenu
Maelezo ya hapa yanakaribia
kufanana na hayo hapo juu kwenye kipengele namba nane (8). Ni uamuzi wenu
kuchagua mnataka sheria ipi itumike kusimamia mkataba wenu. Hii itakuwa ina
nafasi sana kama mnaingia mkataba unaohusisha raia wa nchi zaidi ya moja.
10.
Mambo yatakayopelekea mkataba kuvunjika
Mnaweza mkaweka kifungu ambacho kinabeba
mambo ambayo kama yakifanyika yatapelekea mkataba wenu kuvunjika. Ni vyema kila
upande kwenye makataba ukaguswa kwa namna yake na mambo hayo. Kwa mfano, mnaweza
kukubaliana ya kwamba mnunuzi kama akichelewa kufanya malipo kwa muuzaji kwa
kipindi cha siku thelathini (30) basi atakuwa amevunja masharti mkataba
automatic.
11. Taarifa
Mnaweza pia mkaweka kifungu ndani
ya mkataba ambacho kinatoa anuani ya kutumia taarifa na endapo kama ikitokea
kuna taarifa yoyote ambayo inatakiwa kumfikia yeyote anayehusika na mkataba.
Mnaweza mkaweka anuani ya sanduku la barua au barua pepe au namba ya simu kama
mtakavyokubaliana kwa kila upande.
12. Mkataba unatakiwa usainiwe na wahusika katika
mkataba
Kusaini mkataba ni ishara ya
kwamba wahusika wote katika mkataba wamekubali kufungwa na yaliyomo ndani ya
mkataba. Kabla hujasaini mkataba wowote sana sana ile inayoandaliwa na upande mmoja
‘standard form contract’ mfano wa ile tunayoiombea mikopo Benki uisome kwanza
kwani kusaini mkataba kuna maana kubwa sana kuwa umekubali kubanwa na masharti
yaliyomo ndani kama nilivyokwisha kuelezea, huwezi kusema baadae jamani
sikusoma! utabanwa hata kama hukuusoma.
13. Mashahidi nao wanatakiwa kusaini
Hawa ni vizuri wasipungue wawili
yaani mmoja kutoka kila upande. Hawa kazi yao ni kuthibitisha ya kwamba mkataba
huu umesainiwa na wahusika mbele yao. Mashahidi wanatakiwa wawe ni watu wenye
vigezo vya kuwa mashahidi yaani wasiwe watoto au watu wenye upungufu wa akili
wakati wa kusaini mkataba.
Angalizo: Hivyo nilivyoviaja hapo juu ni mfano wa mambo yale muhimu
yanayotakiwa katika mkataba, hivyo basi pande husika katika mkataba mnaweza kukubaliana
mnavyotaka isipokuwa vipengele vyenu visiende kinyume na sheria za nchi. Pia
ijulikane ya kwamba mikataba inatofautiana. Ni wazi mkataba wa kuuziana gari hauwezi
kufanana na ule ya kuuza au kukodisha nyumba. Kwa maana hiyo nilichokifanya
hapa ndugu msomaji wangu ni kukupa mwanga namna mkataba unatakiwa kuandikwa
vingine utajiongeza.